Monday, May 03, 2021

Kutafakari (Meditation)

Mimi sio mwanasaikologia hivyo sitaandika kama mmoja wao ila nitaandika kuhusu meditations kutokana uchunguzi niliofanya na uzoefu nilionao.

Nilianza kufahamu kuhusu meditations kama miaka 15 hivi iliiyopita. Nilitambulishwa na boss wangu mmoja ambaye alikuwa ni mwenye asili ya kihindi. Alikuwa yeye anaweza kutulia katika situation yeyote. Hata jambo liwe ni la aina gani yeye alikuwa anabakia kuwa mtulivu sana. Ndio siku moja katika kuongea akaniambia yeye anafanya meditation kila siku asubuhi na wakati mwingine hufanya asubuhi na usiku. Wakati huo kulikuwa hakuna information nyingi kama ilivyo sasa hivi hivyo alinipa kitabu.  

Nilikisoma kitabu hicho na kuanza kufanya pole pole ila yeye alichoniambia au alivyokuwa anafanya ni kukaa na kuwasha mshumaa na kuangalia ule mshumaa kwa makini bila kufikiria kitu kingine (focus). Hivyo nilikuwa nafanya wakati wa usiku na kuzima taa na kuangalia huo mshumaa tu. Aliniambia nianze kwa dakika moja na baada ya muda niendelee kuongeza muda. Nilikuwa nafanya kwa muda wa dakika tatu au tano tu.

Nilifanya hivyo ila nilijikuta nasahau kufanya siku zingine. Yaani kwa ufupi sikuiweka meditation kama sehemu ya ratiba ya kila siku. Ila nilipokuwa  mjamzito kama mama kwa mara ya kwanza kuna programs nyingi mtu akipenda anajiandikisha. Hivyo mimi nilijiandikisha na kwenda kufanya yoga ila tukaanza kufundishwa umuhimu kufanya meditations tena. Hivyo kila siku pamoja na mazoezi mengine ila nikawa nafanya meditations. Mimi ni mtu muoga sana na nina wasiwasi sana ila hakuna kipindi katika maisha yangu niliweza  kuwa mtulivu kama kipindi hicho. Kila nikienda kwa clinic nilikuwa nipo sawasawa kabisa nikipimwa blood pressure ilikuwa ipo sawa. 

Hivyo nilifanya meditations kila siku katika kipindi chote nilichokuwa mjamzito na pia mwaka na nusu hivi baada ya kujifungua.Ila kwa vile nilikuwa sijaelewa umuhimu wa meditation au sikuappreciate nikajikuta naanza taratibu kusahau tena kufanya. 

Sasa covid ilipoanza na lockdown ikachangia watu wengi sana hapa kuanza kuwa na depression au anxiety. Kanisani mchungaji akawa anazungumzia sana jinsi watu wanavyomweleza wanavyosumbuluwa na depression na anxiety. Na mimi wakati wa winter nikajikuta kitu kidogo tu kinanipa wasiwasi. Habari za misiba inayosababishwa na covid nchini Tanzania nayo ikaniongezea wasiwasi sana. Hivyo nikaanza kuona katika kila mkutano ninaoshiriki  tunaanza au kumaliza kwa kufanya meditation. Kanisani wakaleta mtu akafundisha "Christian meditation". Siwezi kusema kuwa niliona tofauti zaidi ya kutumia maneno yaliopo katika bible wakati wa kufanya meditation.

Hivyo nikajikuta narudi kufanya meditation tena. Na kitu ninachokiona ni kuwa nimebadilika na kuwa calm kwa mapema sana. Nimejikuta naweza kuchambua au kuchukua muda wa kupumua kabla sijafikia kwenye uamuzi ya kitu fulani. Wasiwasi niliokuwa nao ukapungua sana. 

Kwa vile sasa hivi kuna maelezo mengi sana online kuhusu meditations ikawa ni rahisi sana kwangu kujua tofauti za meditations na njia ya kufanya meditation. Hivyo ikanisaidia sana kuona mafanikio mapema zaidi.